Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Monday, January 21, 2013

Miss Kigoma asaidia wenye ulemavu

Miss Kigoma Anna Wilbroad

MREMBO wa Mkoa Kigoma kwa mwaka 2012/2013, Anna Wilbroad ametoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa watoto wenye ulemavu wanaotarajia kuanza masomo ya shule ya msingi katika kituo maalumu cha walemavu Kabanga kilichopo wilayani Kasulu mkoani Kigoma.

Mrembo huyo alitoa msaada huo wakati wa hafla ya kuwaaga watoto hao walioondokea kwenye ofisi za manispaa ya Kigoma ambapo katika msaada wake pamoja na vitu vingine alitoa sabuni za kufulia, sabuni za kuogea na mafuta ya kupaka kwa watoto hao.

Akizungumza wakati akikabidhi vifaa hivyo kwa watoto hao mrembo huyo ameitaka jamii kujali katika kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu na hasa kuona umuhimu wa kuwasaidia kupata elimu.
Kwa upande wake Mratibu wa mashindano ya Miss Kigoma kutoka kampuni ya Samina Arts, Jumanne Gange alisema kuwa baada ya hafla hiyo pia wanayo mipango mingine kwa ajili ya shughuli za mrembo huyo.
Gange alisema kuwa wanatarajia kuzunguka maeneo mbalimbali ya wilaya za mkoa wa Kigoma kwa ajili ya kufanya sughuli za kijamii kabla ya mrembo huyo kumaliza muda wake na kukabidhi taji.

Awali Ofisa elimu shule za msingi katika Manispaa ya Kigoma Ujiji, Shomari Bane alisema kuwa watoto wanane wamepatikana katika mchakato wa kuwakusanya watoto hao ambao muda huu walitakiwa kuwa shuleni lakini wapo mtaani wakiomba fedha kutoka kwa wasamaria wema.

Bane alisema kuwa zoezi hilo ni endelevu na kwa sasa manispaa yake imeliangalia suala la kuweka bajeti kwa mwaka ujao wa fedha kuhakikisha watoto zaidi ambao wamekuwa wakizurula mitaani wanachukuliwa na kupelekwa kwenye kituo hicho kwa ajili ya kupata elimu.

No comments: