Buchafwe: Nimebuni mashine ya kutengeneza sabuni za mche Mashine
ya kutengeneza sabuni iliyobuniwa na George Buchafwe.
TANZANIA
imejaa wabunifu na wagunduzi, wanabuni zana, vifaa, mashine na vitu vikubwa
ambavyo kama wangewezeshwa kirasilimali
wangechangia vikubwa katika sekta ya sayansi na teknolojia nchini.
Tume ya Sayansi na Teknolojia (Costech), imeanzisha mtindo
wa kutoa tuzo kwa wabunifu mbalimbali. Kama
sio Tuzo ya Mafanikio katika Sayansi na Teknolojia (TASTA) 2011, inayotolewa na
Costech, isingekuwa rahisi kubaini kipaji cha ubunifu alichonacho George
Buchafwe.
Buchafwe ni miongoni mwa mbunifu wanaovuma ambao wapo kwani
ndiye mbunifu wa mashine ya kutengeneza sabuni za mche. Mashine yake imekuwa
kivutio kikubwa katika maonesho ya Sabasaba na Mnazi Mmoja na mahali pengine.
Mashine iliyobuniwa na Buchafwe inatengeneza sabuni za mche kutokana na matunda
ya michikichi yanayoitwa mawese.
Sabuni za mche zinazoitwa Laiki zinatengenezwa katika
mashine yake karakana ya Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO) katika eneo la
Vingunguti mkoani Dar es Salaam. Kipaji cha ubunifu alichonacho ni kikubwa,
anasema atakitumia katika kuwakomboa wajasiriamali. Mashine hiyo aliigundua
mwaka 1991, wakati akifanya kazi katika viwanda viwili vya kutengeneza sabuni.
Alifanya kazi katika kiwanda cha Putwa and Sons kama
mwajiriwa na cha Bob katika muda wa ziada, vyote vikiwa Chang’ombe, Dar es Salaam.
Kilichomsukuma kubuni mashine hiyo, ni kitendo cha kukerwa na tabia ya wamiliki
wa viwanda hivyo kuagiza mashine hizo ughaibuni, Malaysia. Akafikiria kwanini
haiwezekani kutengeneza mashine hapa nchini, akafanya majaribio.
Mwaka mmoja baadaye, akafaulu kutengeneza mashine ya kwanza
na ikaanza kufanya kazi. Ubunifu wake ulionesha mafanikio makubwa kutokana na
rasilimali ya mawese kupatikana nchini na nyingine kuagizwa Malaysia. Kwa
sababu alikuwa mwajiriwa, mashine hiyo waliitumia waajiri wake Wahindi ambao
ndio walikuwa wamiliki wa viwanda hivyo.
Hivyo alipewa nafasi ya kutengeneza mashine nyingi zaidi
zikasambazwa kwenye viwanda vya Wahindi watengeneza sabuni. Miongoni mwa
waliofaidi mashine hizo ni pamoja na kiwanda cha sabuni cha Osman, Fida Hussein
na Jesa. Kupendwa kwa mashine zake, kulimpa hamu Buchafwe ya kuacha kazi,
akaamua kujishughulisha na ubunifu huo wa mashine kwa faida yake.
Baada ya kuacha kazi mwaka 2003, alianza kuhaha kutafuta
mtaji wa kuanzishia karakana ya kutengeneza mashine za kutengeneza sabuni.
Miaka miwili baadaye, alipata mkopo wa milioni mbili kutoka kikundi cha Akiba
na Mikopo cha Kanisa la Africa Inland Church
(AIC), Chang’ombe, Dar es Salaam.
Mtaji ulikuwa mdogo, hivyo haukumpa mafanikio makubwa, hivyo
alikopa mkopo mwingine wa Sh milioni tisa ambao ulimsaidia pia kuanzisha
Kampuni ya Star Natural Product. Buchafwe baada ya kupata mkopo akaanza rasmi
kazi ya kutengeneza mashine. Mashine hizo zilitengenezwa kutokana na vyuma na
mabati yaliyokunjwa.
Ili kufanya kazi, mashine
hizo zilihitaji mota ambazo zilinunuliwa madukani kati ya Sh 800,000 hadi Sh
900,000. Bei za mota zinapishana kutokana na ukubwa, uwezo na ubora wake. Mota
ndogo zinakuwa na supapawa wa saba na kubwa 15. Gharama za mashine
anazotengeneza zinapishana kuanzia hiyo ya Sh milioni nane hadi Sh milioni 20,
hiyo inatokana na matumizi ya umeme.
Ndogo zinatumia umeme wa kawaida nyumbani, lakini kubwa
zinatumia umeme mkubwa wa viwandani, ndiyo maana bei ni kubwa. Kupatikana kwa
vifaa hivyo, kulimfanya ajikite katika kutengeneza sabuni za mche na za maji
kiasi. Kwa kutambua ubunifu wake, Sido waliamua kumchukua na kumpa nafasi ya
kushiriki katika maonesho ya SabaSaba tangu mwaka 2007 katika Viwanja vya
Mwalimu Nyerere.
Akiwa Sido miaka mitatu baadaye, alipewa heshima ya
kusimamia Mpango wa Kuamsha Mawazo ya Wabunifu kwenye shirika hilo. Mashine zilizobuniwa na Buchafwe, ni
imara, bora na zinapendwa na wajasiriamali wadogo wengi jijini na nje ya Dar es
Salaam. Ili kujihakikishia upatikanaji wa
malighafi ya mawese, alipita maeneo inakolimwa Kyela, Ifakara na Kigoma, kutoa
elimu ya uzalishaji bora.
Lakini pia kupitia shirika la Sido walitoa mashine za
kukamua mawese tayari kutumika katika kutengenezea sabuni. Malighafi hiyo ya
mawase kutokana inakopatikana Ifakara, Kyela na Kigoma, inasafirishwa kwenye
mapipa. Ikifikishwa kiwandani Sido, inaingizwa kwenye pipa/mtungi mkubwa wa
kuchanganyika na mixer.
Humo inachanganywa na mafuta na madini yanayoitwa Sodium
Hydroxide. Mchanganyiko huo unazalisha uji mzito ambao kabla ya kutengenezwa
sababu unakaushwa. Uji ukikaushwa, unasagwa katika vipande vidogo vinavyoitwa
nudo (au chipsi) ambazo zikiingizwa kwenye kinu cha mashine hiyo zinasagwa na kutengenezwa
sabuni ya mche.
Mahali inapotengenezwa sabuni panaitwa mode, ndipo mahali
umbo la sabuni na maandishi huandikwa, kadiri mtengenezaji anavyotaka. Hatua
hiyo inahusu sabuni za kufulia, kwa sabuni za kuogea, mchanganyiko huwa na vitu
vingi zaidi. Pamoja na mawese, huchanganywa pia parachichi, ukwaju na jatrofa.
Mchanganyiko huo hufanyika kabla ya kufika kwenye mode
ambapo maumbo ya sabuni hufanyika, liwe miraba au mviringo au namna nyingine
yoyote. Mashine hiyo inaweza kutumia pipa moja au mawili ya mawese kwa siku moja
na ina uwezo wa kutengeneza katoni 30 hadi 100 sa sabuni kwa siku moja, maadam
umeme upo.
Sabuni hizo zinauzwa kwa Sh 8,000 kwa katoni moja na mche
unauzwa Sh 1,000. Kila mtu anaweza kununua mashine hiyo na anapewa miezi sita
ya matazamio. Wanunuzi wengi wanatoka Iringa, Mbeya, Mwanza, Dar es Salaam na Arusha. Buchafwe anakusudia
ifikapo 2015, kusambaza mashine hizo katika mikoa mingi zaidi ya mikoa 10
nchini.
Watu wanafunga nyumbani na viwandani. Mashine hizo tayari
zimevuka bahari na kufika kisiwani Pemba,
ambako sasa zinatumia masalia ya karafuu kutengeneza sabuni. Mashine hizo
zimeongeza ajira kuanzia wazalishaji malighafi, wanunuzi na watengenezaji
sabuni.
Fundi rangi Sido, Koba Hassan anasema, amekuwa mashine hizo
ni mkombozi wa wajasiriamali wadogo kwa wakubwa. Mmoja wa wajasiriamali kutoka Bukoba, Lydia
Paulo anasema, anaomba msaada kwa wafadhili wili apate fedha kwa lengo la
kununua mashine hiyo ambayo itamkomboa kiuchumi.
Buchafwe anatoa mwito kwa Watanzania kuitumia Sido katika
kupata mashine mbalimbali kama yake ya
kutengenezea sabuni. Lakini pia watumie shirika hilo
katika kupata elimu ya ubunifu kwa ajili ya maendeleo ya maisha yao. “Sido inalenga
kuboresha maisha yao.”
No comments:
Post a Comment