Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Wednesday, June 19, 2013

Mbunge wa Kasulu Moses Machali atupiana maneno na Mwenyekiti wa Bunge

Mh. Moses Machali 

MBUNGE wa Kasulu, Moses Machali (NCCR Mageuzi) jana alijikuta akitupiana maneno na Mwenyekiti wa Bunge, Jenista Mhagama bada ya kumtaka Naibu Waziri wa Fedha, Janet Mbene awe na nidhamu, kutokana na kitendo chake cha kutoa ishara ya kumdharau kwa mkono.

Wakati Machali akichangia hoja katika Bajeti ya Serikali jana, Mbene alitoa ishara hiyo ambapo mbunge huyo wa NCCR-Mageuzi aliiona; na kumtaka Naibu Waziri huyo awe na nidhamu na waheshimiane, kauli iliyomuudhi Mhagama na kulazimika kuikemea.
“Machali acha kuropoka, elekeza hoja yako kwa Kiti na kama hutaki kuendelea kaa chini, nimuite mbunge mwingine aendelee,” alisema Mhagama.

Akijibu kauli hiyo ya Mhagama, Machali alisusa na kusema ndio hataki kuendelea tena kuchangia bajeti hiyo na kumwambia Muhagama kuwa na yeye ametumia neno kuropoka, linaloudhi hivyo na yeye Mwenyekiti aache kuropoka vile vile.

Kabla ya kuzuka kwa malumbano hayo, Machali alianza kujadili Bajeti ya Serikali kwa kusisitiza kauli yake ya juzi kumtaka Msajili wa Vyama vya Siasa, kufuta CCM na Chadema kwa kusababisha vurugu nchini.

Katika hoja hiyo, Machali alisema kama kuna vurugu, hakuna uchumi na kutaka vurugu zilizotokea Arusha na Iringa, kama itabainika vyama hivyo vilihusika, hatua zichukuliwe, ikiwezekana kwa kufuta vyama hivyo.

Alitaka CCM na Chadema vijisahihishe, la sivyo kutokana na vurugu zinazoendelea, vyama hivyo vitabakia kuuguza ndugu zao badala ya kuwapa fursa za kwenda katika uzalishaji.

Alisema baadhi ya wanasiasa, wanatumia fursa walizonazo vibaya na kusababisha watu washindwe kuzalisha na kuongeza kuwa hakutakuwa na uchumi kama hakuna utulivu.

Machali pia alizungumzia kodi mpya ya asilimia 14.5 kwa huduma zote za simu, ikiwemo za M-Pesa, Tigo Pesa na Air Tel Money, kwamba ni kuwaonea wananchi.

No comments: