Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Monday, July 8, 2013

Mchungaji kwenda jela miaka 3 Kigoma

MAHAKAMA ya Mwanzo Ujiji iliyopo katika Manispaa ya Kigoma Ujiji, imemhukumu kifungo cha miaka mitatu jela Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste la mjini Kigoma, Jackson Clement maarufu kama Msambya kwa kosa la kuharibu mali.

Akitoa hukumu ya kesi hiyo, Hakimu mkazi wa mahakama ya mwanzo Ujiji, Japhet Manyama alisema amemhukumu mchungaji huyo kifungo jela au kulipa faini ya shilingi 100,000 kutokana na mshitakiwa kuonekana kutenda kosa hilo kwa kukusudia.

Akisoma mwenendo wa kesi kabla ya kutoa hukumu Hakimu Manyama alisema kuwa Oktoba 26 mwaka 2012 mshitakiwa aliharibu kwa makusudi msingi wa nyumba ya Cosmas Paschal Nchunga wakati akijua kuwa kitendo alichokifanya ni kosa kisheria.

Hakimu Manyama alisema awali kulikuwa na kesi ya mgogoro wa kiwanja ambao uliamuliwa katika baraza la nyumba kata ya Gungu na mlalamikaji kuonekana kuwa ni mmiliki halali wa kiwanja hicho ambapo hata hivyo mshitakiwa hakutaka rufaa kupinga hukumu hiyo.

Sambamba na hilo hakimu huyo mkazi alisema kuwa shauri hili lilipelekwa kwenye vikao vya usuluhishi na mlalamikaji kupewa ushindi na kwamba ni jambo la kushangaza kuona kiongozi wa kiroho akiingia kwenye eneo la watu na kuharibu mali.

Katika hukumu yake Hakimu Manyama alisema pamoja na hukumu hiyo mshitakiwa atatakiwa kulipa kiasi cha Sh 200,000 ambazo ni gharama ya msingi wa mali ya mlalamikaji na kutorudi au kurudi tena katika kiwanja hicho cha mlalamikaji.

Akizungumza na gazeti hili Mlalamikaji katika keshi hiyo, Cosmas Nchunga alisema mahakama imetenda haki na amepewa haki yake anayostahili kwani mchungaji huyo amekuwa akimsumbua kuhusu kiwanja hicho licha ya kila mahali wanapoenda kumshinda.

Awali kabla ya hukumu hiyo Mchungaji Clement aliiomba mahakama kumuonea huruma na kumuachia huru kwani yeye ni kiongozi wa familia ya mke mmoja na watoto saba ambapo kuna watoto wanasoma na wanamtegemea yeye kwa mahitaji yao yote ya shule.

No comments: