USAFIRI na usafirishaji bidhaa kwa wananchi katika maeneo
mbalimbali nchini unatarajiwa kuboreka na kuwa nafuu baada ya madaraja 10
yaliyoahidiwa na Serikali kukamilika.
Madaraja hayo yaliyoahidiwa wakati wa kampeni
ya urais kupitia Ilani ya Uchaguzi ya CCM mwaka 2010 ambayo yanagharimu
mabilioni ya shilingi ujenzi wao unakaribia kukamilika.
Hayo yamethibitishwa na Rais Jakaya Kikwete na kuongeza kuwa
kati ya madaraja hayo ambayo thamani yake inakaribia Sh bilioni 415, mawili
tayari ujenzi umekamilika.
Madaraja hayo ni Ruhekei lililoko
Mbinga, Ruvuma na Mwatisi la Morogoro.
Alitoa uthibitisho huo juzi wilaya
hapa wakati akizindua ujenzi wa daraja la Mbutu na kutaja madaraja
yanayoendelea kujengwa kuwa ni Kigamboni, Dar es Salaam kwa Sh bilioni 214.6 na
la Kikwete katika Mto Malagarasi, Kigoma kwa Sh bilioni 90.185.
Mengine ni Kilombero, Morogoro la Sh
bilioni 53.214 na Rusumo mkoani Kagera kwa Sh bilioni 31.7, Sibiti, Singida la
Sh bilioni 17.5, Nangoo, Mtwara Sh bilioni 4.29 na Maligisu, Mwanza, kwa Sh
bilioni 2.51.
Rais Kikwete alisema: “Madaraja
niliyotaja ujenzi wake ukikamilika, tutakuwa tumetimiza ahadi yetu ya kujenga
madaraja yote yaliyotajwa katika Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2010 isipokuwa la
Ruhuhu ambalo maandalizi yake ya ujenzi yanaendelea.”
Alisema baadhi ya madaraja
yanayojengwa sasa na Serikali yalipangwa kujengwa katika Mpango wa Pili wa Taifa
wa Maendeleo mwaka 1968 lakini kwa bahati mbaya hayakujengwa.
Madaraja hayo ni la Kigamboni, Kirumi
kwenye Mto Mara, Rufiji, Kilombero na la Kikwete.
Awamu ya kwanza ilijenga daraja la
Kirumi, awamu ya pili ilifanya maandalizi na awamu ya tatu ikajenga Rufiji na
ya sasa inajenga madaraja matatu yaliyobaki – Kilombero, Kigamboni na Kikwete.
Daraja la Mbutu lina urefu wa
kilometa tatu na linajengwa katika bonde la Mbutu na litaunganisha mikoa ya
Tabora, Singida, Simiyu na Shinyanga na litakuwa na daraja moja kubwa la meta
60 na madaraja mengine madogo saba na hivyo kufanya urefu wa daraja lote kuwa
na mita 165.
Mpaka sasa asilimia 45 ya ujenzi wa
daraja hili lenye thamani ya Sh bilioni 11.28 umekamilika na inakadiriwa kuwa
litakuwa tayari ifikapo Novemba mwaka huu.
No comments:
Post a Comment