Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Monday, December 31, 2012

Warundi 48 ‘waliozamia’ wakamatwa

Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Fraiser Kashai

 
POLISI mkoani Kigoma imewatia mbaroni watu 48 wanaoaminika kuwa ni raia kutoka Burundi ambao walikuwa wakiishi nchini isivyo halali.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Fraiser Kashai aliwaambia waandishi wa habari mjini Kigoma jana kwamba watu hao walikamatwa katika maeneo mbalimbali ya mkoa katika kipindi cha wiki mbili zilizopita.
Kamanda Kashai alisema kukamatwa kwa watu hao kunatokana na msako uliofanywa kwa pamoja kati ya Polisi na maofisa wa Idara ya Uhamiaji katika wilaya zote za mkoa huo.

Kutokana na hali hiyo, Kamanda huyo alitoa mwito kwa wananchi mkoani humo kutoa taarifa kwa vyombo vya ulinzi na usalama wanapowaona watu katika maeneo yao ambao wanatiliwa mashaka kwamba hawako kihalali au wana dalili za kutenda makosa ya kihalifu.

Katika tukio lingine, mtoto wa miezi sita, Amina Athumani anayeishi Kibondo, amekufa baada ya kuungua na moto ulioteketeza nyumba waliyokuwa wakiishi ambapo katika tukio hilo, dada yake, Agnes Ayubu alinusurika kifo na kujeruhiwa vibaya na moto huo.

Kamanda Kashai alisema chanzo cha moto huo ni mshumaa uliowashwa na mama wa watoto hao, Neema Stefano ambaye baada ya kuwasha mshumaa huo, aliuacha ukiwaka na kwenda dukani kupata mahitaji mengine na ndipo mshumaa huo ulidondoka na kusababisha moto mkubwa ulioleta maafa.

Kwa sasa, Kamanda Kashai alisema Agnes amelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kibondo kwa matibabu huku mama huyo akishikiliwa na polisi kwa mahojiano zaidi na uchunguzi wa tukio hilo unaendelea.



No comments: