MRATIBU wa Ukimwi katika Manispaa ya Kigoma/Ujiji, Exavery
Kehegwa na aliyekuwa Mhasibu wa Manispaa hiyo, Christina Nyamahinzu
wamepandishwa kizimbani kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Mahakama ya Wilaya
Kigoma na kusomewa mashitaka mawili ya kula njama za kuiibia Serikali na
kumdanganya mwajiri.
Mbele ya Hakimu mkazi wa Mahakama hiyo, David Ngunyale
Mwendesha Mashitaka kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru),
Moses Malewo alisema kuwa watuhumiwa hao walitenda kosa hilo wakati wakijua kufanya hivyo ni kosa
kisheria.
Ilielezwa mahakamani hapo kwamba watuhumiwa wanadaiwa
kuandika taarifa wakieleza kuwa Oktoba 9 mwaka 2010 waliandaa semina ya siku
mbili ya Ukimwi kwa wadau 22 wa manispaa hiyo huku kila mjumbe akilipwa Sh
20,000 kwa siku wakati si kweli.
Kwa mujibu wa Mwendesha Mashitaka huyo kutoka Takukuru,
watuhumiwa wanadaiwa kufanya kosa hilo
kinyume na kifungu namba 22 cha sheria ya makosa ya adhabu.
Watuhumiwa wote walikana makosa yao na kwamba kesi hiyo itaitwa tena
mahakamani hapo Oktoba 9 mwaka huu ambapo hoja za awali kwa watuhumiwa
zitawasilishwa.
No comments:
Post a Comment