Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Monday, August 6, 2012

Zitto- Sina bei na sitasalimu amri


Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema)
MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema), amepinga tuhuma za rushwa dhidi yake na kusema kuwa, yeye hana bei, hajawahi kuwa na bei na kamwe hawezi kusalimu amri katika mapambano dhidi ya rushwa.

Zitto amesema, kuna njama za kumdhoofisha na kumvunja moyo katika mapambano dhidi ya rushwa hivyo ameomba vyombo vya Dola vichunguze ili kupata ukweli na endapo itathibitika alihongwa yupo tayari kuwajibika.

Sitasalimu amri mbele ya dhamira zao ovu hata nitakapobaki peke yangu katika mapambano hayo ya kulinda na kutetea rasilimali za taifa zinufaishe watanzania wote” amesema Zitto leo wakati anazungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma.

Naamini katika nchi yetu tunazo rasilimali za kutosha mahitaji/haja ya kila mmoja wetu lakini si ‘tamaa/ulafi’ wa baadhi ya watanzania wenzetu” amesema Mbunge huyo kijana ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Zitto amesema, hivi sasa kuna tabia ya kuwamaliza wanasiasa wenye kudai uwajibikaji na uzalendo, na kwamba baadhi ya mbinu hizo chafu zimewahi kumlenga yeye lakini anaamini zitashindwa.

Kumeanzishwa kiwanda kwenye medani ya siasa cha kuzalisha majungu na fitna zenye lengo la kuwachonganisha wanasiasa wa aina hiyo na wananchi kwa kutumia vyombo vya habari na nguvu ya fedha.Naamini mbinu hizi chafu, kama nyingine nyingi zilizojaribiwa kwangu huko nyuma nazo zitashindwa” amesema.

Zitto amesema, kama ikithibitika kuwa alihongwa, yupo tayari kuhukumiwa, na kujiuzulu uenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mashirika ya Umma (POAC).

Mimi Zitto Zuberi Kabwe sina bei, sijawahi kuwa nayo na sitarajii kuwa nayo huko mbeleni. Daima nimesimamia kidete maadili ya uongozi bora katika maisha yangu yote ya siasa, na nawaahidi sitarudi nyuma katika mapambano dhidi ya rushwa katika nchi hii pamoja na mikakati ya aina hii ya kunidhoofisha na kunivunja moyo” amesema Zitto. Amehoji kwa nini POAC inahojiwa kwa ajili ya Tanesco tu wakati kama hiyo inasimamia mashirika ya umma 259 na kwamba hicho ni kitendawili.

Mchango wa Kamati hii katika Bunge na kwa ustawi wa Mashirika ya Umma ni bayana na haujawahi kutiliwa shaka. Kamati yetu imeokoa upotevu mkubwa wa mali za umma na kuokoa fedha za umma kutokana na umakini wake. Tumefanya hivyo CHC hivi karibuni, Kiwira na kwenye mashirika mengine mengi. Kote huko uadilifu na uzalendo wa Kamati hii haujawahi kuhojiwa. Inatuwia vigumu kuona kuwa tunahojiwa katika suala hili la Tanesco. Hapa pana kitendawili.” amesema Zitto.

Amesema, kuna hoja zinazopandikizwa kutaka POAC ivunjwe na haswa zikimlenga yeye, na kwamba anaelewa kiu ya wasioitakia mema nchi hii hivyo wahusika wanataka ivunjwe au sura zibadilishwe kwa kuwa maelezo kuwa Kamati hiyo imekuwa mwiba kwa mikakati yao ya kifisadi.

Kwa maoni yangu, Kamati ya POAC isihusishwe na tuhuma hizi kwa vyovyote vile. Niko tayari nihukumiwe mimi kama mimi na sio kuhusisha wajumbe wengine ambao hawatajwi mahala popote katika tuhuma hizi mbaya sana katika historia ya Bunge letu. Nitakuwa tayari kunusuru Kamati ya POAC na maslahi ya taifa letu kwa kujiuzulu Uenyekiti iwapo itathibitika pasipo shaka kuwa nimehongwa.Kamati ya POAC ni muhimu zaidi kuliko mimi.” amesema Zitto.

Amedai kuwa, kuna wanasiasa hasa wa Upinzani wanaoutaka Uenyekiti wa POAC na wanafanya kila njia kutaka kuidhoofisha.
Msishangae pia kuja baadae kubaini kwamba baadhi ya wanasiasa wenye midomo mikubwa ya kutuhumu wenzao wao ndio vinara wa kupokea rushwa.” amesema Mbunge huyo ambaye pia ni Naibu Kiongozi wa upinzani bungeni.

Nafahamu nabeba dhamana kubwa ya uongozi, taswira yangu ya uongozi daima imeakisi njozi na matumaini ya wananchi wa Kigoma Kaskazini, wananchi wanyonge na vijana kote nchini bila kujali itikadi zao za kisiasa, jinsia zao, makabila yao na rika zao. Hivyo, nawajibika kupitia kwenu kuwatoa hofu juu ya hisia potofu zinazopandikizwa kwao na wale wasiopenda kuona baadhi yetu tukiwaunganisha na kuwasemea watanzania wasio na sauti, dhidi ya vitendo vya hujuma na vyenye dhamira ovu kwa taifa.” amesema Zitto.

No comments: