POLISI mkoani Kigoma inawashikilia watu watatu wakiwemo
wafanyakazi wawili wa basi la Osaka linalofanya safari kati ya Kigoma na Dar es
Salaam, wakituhumiwa kufanya biashara haramu ya kusafirisha watu hai.
Kamanda wa Polisi Mkoa Kigoma, Fraiser Kashai aliwaambia
waandishi wa habari mjini hapa kwamba juzi saa 10 jioni askari wa upelelezi
wakiwa katika doria, waliona basi la abiria katika kijiji cha Heru Juu wilayani
Kasulu likikusanya watu kwa ajili ya kuwasafirisha.
Alisema katika kufuatilia hayo askari
hao wa upelelezi waligundua basi hilo lilifika kijijini hapo kwa ajili ya
kuwachukua abiria 44 ambao walikuwa katika mpango wa kuwasafirisha kuwapeleka
Msumbiji kwa ajili ya kwenda kufanya kazi za kukata mbao.
Katika tukio hilo Kamanda huyo wa
polisi alisema wanamshikilia mfanyabiashara na mkazi wa jijini Dar es Salaam,
Michael Mgala ambaye ndiye aliyekuwa akihusika na kitendo cha kuwakusanya watu
hao kwa ajili ya kuwasafirisha.
Alisema jeshi hilo pia linawashikilia
watumishi wawili wa basi la Osaka lenye namba za usajili T 481 BFJ, akiwemo
dereva Waziri Hadaike na kondakta wake Erick Mangesho. Kwa sasa polisi
inaendelea kuwahoji watu hao kubaini kosa lao.
Hata hivyo, Kamanda huyo alisema
wamewaachia huru watu hao 44 waliokamatwa katika tukio hilo kwa kile
kinachoonekana kwamba hawana kosa katika hilo kwa vile wao ni waathirika.
No comments:
Post a Comment