Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Sunday, August 12, 2012

Zitto ahakikishiwa manufaa ya urani kwa wanaoizunguka



WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amehakikishia umma kuwa wamejipanga kuhakikisha kwamba madini ya urani yanaleta manufaa kwa taifa kwa kusema uingiaji mkataba hautakuwa kwa mtindo wa zamani ambao haukuleta manufaa kwa wananchi.

Wakati Waziri Muhongo alihakikishia hayo Bunge jana, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema) alitoa tuhuma dhidi ya Kampuni ya Urusi inayotarajiwa kuchimba madini hayo chini ya mradi maarufu unaojulikana kama Mkuju River Project Uranium, kwa kusema inadaiwa na Mamlaka ya Mapato (TRA) takribani dola milioni 186 zilizotokana na mauziano ya kubadilisha umiliki wa mradi husika.

Mwaka jana, Kampuni ya Mantra Resources ya Australia iliuza mradi huu, kampuni nzima asilimia 100 iliuzwa kwenda kwa Kampuni ya Russia ya ARMZ kwa thamani ya dola za Marekani milioni 980, na baada ya mauzo hayo, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) walihitaji walipwe ruzuku ya mapato asilimia 80 mpaka asilimia 20 ambayo ni sawa milioni 186. Mpaka sasa fedha hizi hazijalipwa,” alisema Zitto.


Aliendelea kusema, “Na serikali inafanya mazungumzo na kampuni hii…na si kweli kwamba Kampuni ya Uhuru One ni tofauti na hiyo kampuni ya Urusi, Kampuni ya Uhuru One ni sehemu ya kampuni hiyo ya Urusi... Palitokea mabadiliko ya umiliki wa kampuni hiyo na Serikali inapaswa kuhakikisha kabla ya leseni maalumu ya uchimbaji haijatolewa kwa ajili ya Mradi wa Mkuju River Project Uranium, ipate fedha hizo.

Zitto alitoa taarifa hiyo baada ya Waziri Muhongo kujibu swali la Mbunge wa Mkoani, Ali Khamis Seif aliyehoji ni namna gani Serikali itanufaika na uchimbaji wa urani unaosadikiwa kuanza mwakani.

Akijibu taarifa hiyo ya Zitto, Waziri Muhongo alisema: “nimweleze kwamba leseni haijatolewa na haitatolewa, na hayo anayoongea sisi tunafuatilia zaidi kuliko yeye (Zitto), na asiwe na wasiwasi.”

Awali Mbunge wa Mkoani, Seif alitaka ufafanuzi juu ya kampuni zinazohusika na uchimbaji akisema kampuni iliyofanya utafiti katika mto Mkuju inaitwa Mantra na itakayochimba ni Uhuru One.

Inadhihirisha kuwa kuna biashara baina ya kampuni mbili. Je Serikali itanufaika vipi katika kampuni hiyo,” alihoji mbunge na kutaka ufafanuzi juu ya kama Serikali itakuwa mwanahisa bila kuwekeza, ni gawiwo la asilimia ngapi itapata. “

Hapa kuna Serikali ya Urusi, kuna Uhuru One kama ilivyo sisi tulivyo na Stamico…serikali ya Urusi ndiyo mmiliki wa Mantra Resource, zinabadilika badilika lakini zote ni kampuni zake,” alisema Waziri Muhongo na kujulisha Bunge kwamba juzi walikutana na kampuni hiyo. Alisema katika kikao hicho Serikali ya Tanzania inabadilisha mtindo ambao wananchi hawafaidiki.
Leo (jana) kuna mazungumzo kati ya Stamico, wizara na kampuni juu ya namna ya kupata shares (hisa),” alisema Profesa Muhongo.

Aliendelea kuliambia Bunge kuwa, “niliwaeleza kuwa wao watakuja na fedha na teknolojia na sisi tunakuja na Urani. Sio mtindo wa zamani, mwekezaji anakuja na kusema wewe una nini unasema hatuna kitu.”

No comments: