Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Tuesday, August 21, 2012

Waliyochochea kugomea sensa kufikishwa Mahakamani


WAKATI watu sita wa Mwandiga nje kidogo ya manispaa ya Kigoma Ujiji wakipandishwa kizimbani kusomewa mashitaka ya kuchochea kugomea sensa, Waziri Mkuu Mizengo Pinda ametaka mashehe wanaoendelea kupiga vita sensa waache.

Amesema kufanya hivyo ni kosa la kisheria linaloweza kukwamisha maendeleo ya nchi na kuisababishia Serikali hasara.

Akizungumza wakati wa uzinduzi maalumu wa kampeni ya uhamasishaji sensa ya watu na makazi kwa mwaka 2012 Dar es Salaam jana, Waziri Mkuu alisema licha ya kuwapo watu wachache wanaotaka kukwamisha sensa, Serikali itahakikisha inafanikiwa kwa asilimia 100, kwa sababu imegharimu fedha nyingi.

Alisema, “Watanzania hawana budi kufahamu kuwa sensa ya watu na makazi si kwa ajili ya kujua Waislamu ni wangapi na Wakristo ni wangapi. Nia yetu si kujenga misikiti wala makanisa, hivyo Watanzania wasikubali kurubuniwa na wachache wenye nia mbaya ya kukwamisha mipango ya Serikali katika kuleta maendeleo ya nchi.

Nina taarifa za kuwapo mashehe wachache wanaoendelea kusambaza vijarida na vipeperushi vinavyokataza Waislamu kushiriki sensa. Nashukuru nimevisoma vipeperushi hivyo na kuona jinsi taarifa zilizochapishwa zinavyopotosha. Kwanza chanzo cha taarifa hizo si Serikali wala ofisi ya takwimu, ndiyo maana zinajichanganya na kurubuni watu”.

Kutokana na maelezo yake, mashehe hao wanaostahili kupuuzwa, hawatafanikisha lengo lao kwa sababu idadi kubwa ya mashehe imemhakikishia ushirikiano wa kutosha, kuhakikisha sensa haikwami.

Mtakaofikiwa na mliokwishafikiwa na vipeperushi hivyo, kataeni ushawishi usio na tija kwa kuwa hatujalenga kujua idadi ya waumini wa dini zilizopo nchini wala idadi ya watu pekee. Tunafanya sensa, ili pamoja na sababu nyingine, kujua taarifa zenu kwa ajili ya kupanga mipango ya maendeleo, huku tukitathmini utekelezaji wa dira ya Taifa,” alisema Pinda.

Alifafanua pia kuwa lengo lingine la sensa ni kutathmini utekelezaji wa malengo ya milenia hivyo watu wasiichanganye na mazoezi mengine.

Tangu tulipoanza maandalizi ya sensa mwaka 2004 tulihakikisha eneo la elimu kwa umma linazingatiwa, ili kuwapa watu uelewa wa kutosha. Wasimamizi na makarani wa sensa nao wamepewa elimu ili mambo yaende sawa, lakini hiyo haitoshi, tunategemea viongozi wa dini, vyama vya siasa na wa taasisi watusaidie kusambaza elimu ya umuhimu wa sensa katika siku chache zilizobaki, ili lifanikiwe kwa faida ya wote,” alisema.

Kwa mujibu wa Waziri Mkuu, hadi kukamilika, Sh bilioni 141 zitakuwa zimetumika ambazo vyanzo vyake ni Serikali iliyotoa asilimia kubwa pamoja na fedha nyingine kutoka kwa mashirika wahisani.
Akizungumza wakati wa ukaribisho, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Meck Sadick alisema wameanza kushughulikia suala la mashehe wanaosambaza vipeperushi hivyo, ili wasitishe ‘mchezo’ huo, kwa kuwa unakwenda kinyume na Sheria Namba Moja ya mwaka 2002 inayotaka watu wasinyimwe haki yao ya kuhesabiwa.

Kwa kweli wanadanganya Waislamu na hadi jana jioni (juzi) mashehe hao wachache walikuwa wakipita misikitini na makazi ya Waislamu kugawa vipeperushi vyenye taarifa za kupotosha kuhusu sensa. Tumeanza kushughulikia suala lao,” Sadick alisema.

Mwenyekiti wa Kamati Kuu ya Taifa ya Sensa ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Iddi alisema uelewa wa sensa kwa watu wengi bado ni changamoto kubwa inayohitaji elimu ya ziada. Sensa itakayoanza usiku wa Agosti 25 itakwenda sambamba na uandikishwaji wa watu katika Daftari la Makazi.

Wakati huo huo, watu sita waliofikishwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Kigoma, Emmanuel Mrangu na kusomewa mashitaka na Mwendesha Mashitaka wa Polisi Inspekta Jonas Kakwaya ni Juma Hussein, Shuli Amadi, Khadija Sijali, Yapemacho Hussein, Malundo Mussa na Juma.

Kakwaya alidai mahakamani hapo juzi kuwa huku wakijua kwamba kufanya hivyo ni kosa washitakiwa walishawishi jamii kugomea sensa. Katika kesi hiyo namba 356 ya mwaka huu washitakiwa Agosti 16 eneo la Mgera Mwandiga nje kidogo ya Kigoma Ujiji walibandika karatasi walizochapisha juu ya mabango ya Serikali ya kuhamasisha sensa yakitaka wananchi wakatae kuorodheshwa.

Washitakiwa walikana mashitaka na dhamana kuwa wazi lakini hawakupata wadhamini na hivyo kupelekwa gereza la Bangwe mjini Kigoma hadi Agosti 30, kesi hiyo itakapotajwa. Mwendesha Mashitaka aliiambia Mahakama hiyo kwamba upelelezi haujakamilika.

Katika hatua nyingine, jana kulizuka mgogoro kati ya makarani na wasimamizi wa mafunzo ya ngazi ya Taifa katika Kituo cha Shule ya Msingi ya Buguruni, Dar es Salaam wakidai kulipwa posho zao za siku tano za mafunzo waliyokuwa wakihudhuria. Makarani hao walijikusanya nje ya geti huku wakipiga mayowe ya kutaka haki yao, wengi wao wakionekana kuchoshwa na ahadi ambazo walidai wamekuwa wakiahidiwa na msimamizi mkuu wa semina hiyo.

Leo ni siku ya tano hatujalipwa posho zetu za semina lakini tukiuliza wanatupiga kalenda tu,” walidai baadhi ya makarani hao ambao hawakutaka kutajwa majina.

Msimamizi Mkuu wa Kituo hicho aliyejitambulisha kwa jina la Alphonce Msinduki wa Manispaa ya Ilala alisema wanachosubiri ni matokeo ya mitihani waliyofanya na kuwataka warudi leo kutokana na wasimamizi hao kutingwa na kazi ya kusahihisha mitihani ndipo wawape matokeo na posho, lakini ikawa tofauti.
 (Mkuu wa Wilaya) aliwaambia waondoke waingie darasani, kesho (leo) matokeo yao yatatolewa na kupatikana wenye sifa ambao ndio watalipwa posho,” alisema.</p>
Posho waliyopangiwa ni Sh 35,000 kwa kutwa. Karani mwingine alidai kuwa huenda kukawa na njama za kutaka kuwadanganya ili wachukuliwe wasiofaa kwani waliambiwa waondoke eneo hilo na wawahi leo saa moja asubuhi kusikilizia matokeo. Malalamiko, lawama na kashfa kwa baadhi ya wasimamizi wa mafunzo kudaiwa kutumia fedha za posho za makarani wa sensa katika biashara na miradi binafsi vimeongezeka.

Malalamiko hayo yalilifikia gazeti hili tangu wiki iliyopita, ambapo baadhi ya makarani walidai jana kuwa siku ya sita na wengine ya tano tangu mafunzo yaanze, lakini hawajalipwa posho zao kulingana na makubaliano ya mkataba.

Hapa kwetu tulianza mafunzo Alhamisi iliyopita (Agosti 9) cha kushangaza mpaka leo, hatujalipwa chochote kinyume cha makubaliano ya mkataba, wahusika wanadai Serikali haijatoa hela, lakini baadhi yao tuna taarifa wanatumia fedha hizo kufanya biashara zao, hii si haki,” alidai karani wa Kigamboni, Dar es Salaam ambaye hakuwa tayari kutajwa jina gazetini.

Karani huyo alidai kuwapo vituo vya sensa sehemu zingine Kigamboni, ambako makarani wamelipwa Sh 150,000, wengine Sh 75,000 tofauti na makubaliano ya kulipwa kwa siku Sh 35,000 jambo linalodhihirisha kuwapo ajenda ya siri itakayoigharimu Serikali isipochukua hatua.

Alisema makarani wengine wamevunjwa moyo na wanafikiria kuchakachua sensa ikiwa hali hiyo itaendelea, hivyo kuitaka Serikali ifuatilie na kuhakikisha stahili zao kulingana na mkataba ili kuepusha athari zozote.

Malalamiko yapo pia katika maeneo ya Kibangu, Kimara-Bonyokwa, Mbezi-Temboni na Kibanda cha Mkaa na Tegeta katika Wilaya ya Kinondoni na Keko Machungwa, Mbagala Kuu wilayani Temeke na Kunduchi.

Habari hizi zimeandikwa na Namsembaeli Mduma, Fadhil Abdallah, Fadhil Akida na Gloria Tesha.

No comments: