Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Saturday, July 28, 2012

Zitto aponda mjadala wa urais



MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema) ameeleza kushangazwa na taharuki ambazo watu huzipata masuala ya urais yanapotajwa huku akiasa muda usipotezwe kujadili nafasi hiyo nyeti kwa kuwa katika chama chake, hajajulikana atakayegombea.

Suala la urais lisitupotezee muda, kwani kuna mambo mengi sana ya kujadili kuhusu nchi yetu. Taharuki ambazo watu wanazipata masuala ya urais yanapotajwa, zinashangaza sana,” alisema Zitto katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana.

Katika taarifa hiyo iliyolenga kujiengua na taarifa za hivi karibuni zilizoandikwa juu yake kuhusu suala zima la urais, alisema, “mwanachama wa chama chetu atakayekubalika na jamii na wajumbe wa mkutano wa uteuzi, ndiye atakuwa mgombea wetu. Kwa sasa hayupo na hivyo tusipoteze muda kujadili jambo hili.”

 Msingi wa taarifa hiyo ulilenga kile alichosema asihusishwe na matamshi na makanusho ya wabunge ambao hivi karibuni, walinukuliwa katika gazeti la Mwananchi, wakidaiwa kumsafishia Zitto njia ya urais mwaka 2015.

 Zitto ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, alisema miongoni mwa wabunge hao ni Halima Mdee na Joshua Nassari wote wa Chadema ambao walijitokeza na kusema waliyonukuliwa katika gazeti hilo hawakuyasema.

Mbunge mwingine ni Esther Bulaya wa Viti Maalumu CCM ambaye alitumia juzi mtandao wa jamii wa Facebook kukanusha juu ya kilichoandikwa na gazeti hilo. “Nasikitika sana kuambiwa kuwa nimempigia debe la urais Zitto Kabwe.

Huu ni uongo wa kutupwa; tulikwenda Kigoma kuwaunga mkono wasanii wa Kigoma walioamua kuchangisha fedha za ujenzi wa kituo cha vijana.

Nilikwenda kama mbunge wa vijana kwa ajili ya kuunga mkono vijana wenzangu. Huu ni uzushi mkubwa. Natambua kila chama kina utaratibu wa kupata mgombea urais,” alisema Bulaya kupitia mtandao.
Akitoa ufafanuzi, Zitto alisisitiza kutaka asihusishwe kwa njia yoyote na matamshi yao, habari iliyowanukuu na hata makanusho yao, akisema mwishowe ukweli utasimama.

Alifafanua, kwamba wabunge hao na wengine wengi, hakuwaalika yeye isipokuwa ni vijana wasanii wa Kigoma All Stars na huku yeye akisaidia masuala ya lojistiki.

Alisema lengo la kuwaalika wabunge kutoka vyama mbalimbali lilikuwa ni kuonesha umoja na mshikamano wa nchi bila kujali misimamo ya kisiasa. Licha ya Mdee, Nassari na Bulaya, wabunge wengine ambao Mratibu wa Tamasha, Mwasiti Almasi aliwaalika wakahudhuria ni Kangi Lugola, Deo Filikunjombe, Raya Ibrahim, Amina Mwidau na David Kafulila.

Walioalikwa lakini hawakuhudhuria ni Joseph Mbilinyi, David Silinde, Amos Makala, Vicky Kamata na Peter Serukamba. Kwa mujibu wa Zitto, wote walioalikwa waliambiwa hiyo ni shughuli ya muziki na hakufanya mazungumzo nao kukubaliana nini cha kuzungumza.

Tamasha lilikuwa la muziki na halikuhusika kabisa na siasa. Ni bahati mbaya sana kuwa kuna matamshi ya kisiasa yalitamkwa katika shughuli ile,” alisema na kuongeza kuwa wabunge wote walipewa nafasi ya kusalimia.

Alitaja waliozungumza kwa muda mrefu kuwa ni Mdee, Nassari, Filikunjombe na Lugola. Hata hivyo alisema hotuba za wabunge zilirekodiwa kwenye video neno kwa neno na akaahidi kuziweka wazi kwenye blogu yake. Katika kujiengua zaidi na habari hiyo, Zitto alisema, “kama mwandishi kaandika ambayo wabunge hawakusema basi itaonekana kwenye video hizo.

 Wabunge wenyewe wanajua kwenye nafsi zao nini walisema Kigoma na kipi kiliwasukuma kusema waliyosema Kigoma.” Zitto alisema:“Mzee Thabiti Kombo alituachia wosia tunapokuwa tunazungumza.
Alisema 'weka akiba' si akiba ya fedha, bali ya maneno. Tuweke akiba ya maneno. Tusimalize yote”.

Akichangia hotuba ya makadirio ya matumizi ya Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi bungeni jana, Zitto alisema amesikia maneno mengi baada ya kuunganisha wasanii wenye asili ya Kigoma. Alisisitiza kuwa nia yake ni kuendeleza mkoa wa Kigoma na kutetea maslahi ya wasanii kwa jumla.

Nashangaa watu wanalihusisha na urais! Mungu akitaka mtu awe rais hakuna anayeweza kuzuia. Kwa taarifa yenu, uadilifu wa kuwa Amiri Jeshi Mkuu wa Taifa letu ninao, hata yakisemwa maneno mengi lakini Mungu akitaka hakuna wa kunizuia,” alisema Zitto.

No comments: