Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Saturday, July 28, 2012

Wataokataa kulipa kodi Ujiji kushitakiwa



BARAZA la madiwani la Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji limesema kuwa ushuru unaotozwa kila siku na manispaa hiyo katika masoko yake utaendelea kutozwa na hautafutwa.

Msimamo huo unafuatia kauli ya Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri aliyoitoa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika mjini Kigoma hivi karibuni.

Akitoa majumuisho ya azimio la madiwani, Meya wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Bakari Beji alisema kuwa wananchi hawakuelewa maeneo ya utozaji ushuru kwa wafanyabiashara hao ambayo Naibu Waziri alizungumzia.

Beji alisema kuwa Naibu Waziri huyo alizungumzia wafanyabiashara ndogo ndogo nje ya masoko ya manispaa hiyo na si wale waliopewa meza na vizimba ambao kwa wiki moja sasa wamekataa kulipa ushuru wa Sh 300 kwa kisingizio cha kutekeleza agizo la Naibu Waziri huyo.

 Kutokana na mgomo huo wa wafanyabiashara hao, Meya alisema kuwa kikao cha fedha na uongozi cha manispaa hiyo kilikaa na kujadili kwa kina suala hilo na kufikia uamuzi wa kuwafungulia mashitaka wafanyabiashara watakaokaidi kulipa ushuru huo.

Hata hivyo, alisema kwanza watawaelimisha wafanyabiashara ho nini kilichotokea na kile walichopokea.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Alfred Luanda alisema kuwa waraka wa mwaka 2002 ulikuwa unazungumzia kufuta kodi, ushuru na ada ambazo ni kero kwa jamii na zipo biashara na maeneo ambazo waraka huo umebainisha zifutwe na siyo vizimba na meza za biashara kwenye masoko.

Akizungumza katika kikao hicho cha baraza la madiwani, mkuu wa wilaya Kigoma, Ramadhani Maneno alisema kuwa chanzo cha mgogoro wa wafanyabiashara kukataa kulipa ushuru na kodi ya pango unatokana na wataalamu kushindwa kusimamia kikamilifu mikataba baina ya pande mbili hizo.

No comments: