Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Saturday, September 10, 2011

CHRISTINA SHUSHO: Mtoto wa Kibirizi Kigoma, anayetamaba kwenye Injili

“UNIKUMBUKE Babaa unapowazuru wengine naomba unikumbuke, usinipite Yesu unapowazuru wengine naomba unikumbuke, unikumbuke babaa unapowazuru wengine naomba unikumbuke…”

Haya ni baadhi ya maneno yaliyomo katika moja ya nyimbo zinazomtambulisha vyema Mwimbaji wa Nyimbo za Injili, Christina Shusho.

Shusho amefanikiwa kujijengea sifa kwa mashabiki wa nyimbo za Injili ndani na nje ya mipaka ya Tanzania kutokana na nyimbo zake kubeba ujumbe mzito kwa jamii, lakini ukiwa katika msingi wa neno la Mungu ambalo analiamini.

Umahiri wake katika kuimba nyimbo za Injili umemuwezesha Shusho kutambulika vyema na kujinyakulia Tuzo mbalimbali ikiwemo Tuzo aliyopata wiki chache zilizopita huko Nairobi, Kenya.

Shusho alikuwa kati ya wasanii wa Tanzania waliopata Tuzo za Muziki za Afrika Mashariki na Kati (EMAS) zilizofanyika Agosti 20, mwaka huu na kushirikisha wasanii mbalimbali wa kutoka nchi nane za Afrika Mashariki na Kati.

Mwimbaji huyo aliibuka na Tuzo ya Msanii Bora wa Kike wa Nyimbo za Injili akiingia na wimbo wake Unikumbe na kumshinda mwimbaji mwenzake kutoka Tanzania Upendo Nkone aliyeingia na wimbo wake Haleluya Usifiwe, Alice Kamande kutoka Kenya na wimbo wake Upendo na Gaby kutoka Rwanda na wimbo wake Amahoro.

Mbali na kuwa mwimbaji wa nyimbo za Injili, Shusho anasema anapenda kupendeza na kuonekana maridadi na ndio maana pia anajishughulisha na masuala ya ubunifu wa mavazi na pia ananunua bidhaa au vitu kutoka nje.

Lakini pia Shusho ni mtangazaji wa kituo cha televisheni SIBUKA na akiendesha kipindi kinachojulikana kama Gospel Hits.

Hata hivyo anasema lengo lake ni kuanzisha kipindi chake cha televisheni ambacho anasema atakiita Christina Talk Show na kwamba kitakuwa kikijadili masuala mbalimbali ya kijamii bila kubagua kabila au dini kwani lengo ni kuisaidia jamii ya Watanzania.

Mwimbaji huyo ambaye ni mke wa mtu, wamebahatika kupata watoto watatu anasema amesoma hadi kidato cha nne kisha akasomea masuala ya Teknolojia ya Mawasiliano (IT) katika Kituo cha Kompyuta cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UCC), lakini matarajio yake ni kujiunga na Chuo Kikuu kwa ajili ya kupata elimu zaidi.

“Ndoto yangu Mungu akinisaidia nataka mwakani niingine chuo kikuu na nikitoka huko niwe Daktari wa Taaluma. Lengo langu ni kusomea Uongozi wa Biashara, nataka pia kuchukua kozi ya muziki ili kuongeza ujuzi zaidi,” anasema na kuongeza kuwa anataka kuchukua masuala ya uongozi wa biashara kwa sababu hata muziki, ubunifu vyote vinahitaji usimamizi.
(TUNAKUTAKIA KILALA HERI MAMA)


No comments: