MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Kanda ya Tabora imewahukumu kifungo
cha miaka mitano jela askari saba wa Jeshi la Polisi mkoani Kigoma ambao walikuwa
wakishtakiwa kwa mauaji.
Akitoa hukumu yake katika kikao cha Mahakama Kuu kilichokuwa
kikifanyika mkoani Kigoma Jaji wa mahakama hiyo, Sam Mpaya Rumanyika alisema
kuwa baada ya kupitia ushahidi mbalimbali Mahakama hiyo imewatia hatiani askari
hao kwa kosa la kuua bila kukusudia.
Katika kesi hiyo namba 35 ya mwaka 2012 washitakiwa hao
walifikishwa mahakamani hapo na kusomewa shitaka la kumuua Festo Stephano,
mkulima wa kijiji cha Rungwe Mpya Wilaya ya Kasulu mkoani hapa katika tukio lililotokea
Agosti 6, mwaka 2011.
Askari hao waliohukumiwa ni pamoja na Baraka Hongdi, Koplo
Mawazo, Koplo Swahib, D/C Charles, D/C Shamsi, D/C Jerry na D/C Amrani ambao
kwa pamoja walikana shitaka lao katika kesi hiyo namba 35 ya mwaka 2012.
Akitoa utetezi kabla ya hukumu hiyo wakili wa washitakiwa,
Method Kabuguzi aliiomba Mahakama kuwafutia shitaka washitakiwa hao na
kuwaachia huru kwani wote bado vijana na wameoa hivi karibuni.
Sambamba na hilo Kabuguzi alisema kuwa askari hao walikumbwa
na mkasa huo wakati wakitekeleza jukumu lao la ulinzi wa taifa ambapo
walimkamata mtuhumiwa wa kutumia silaha na ndipo kifo kikatokea wakati
wakitekeleza majukumu yao.
No comments:
Post a Comment