Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Friday, August 9, 2013

'Wamiliki silaha Kigoma,wahamiaji haramu waondoke kabla ya operesheni'



POLISI imetaka watu wanaomiliki silaha kinyume cha sheria na wahamiaji haramu ama kuondoka au kuhalalisha ukazi wao, kabla ya operesheni kamambe kuanza. Taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi hilo, Advera Senso, imetaka wenye silaha wazisalimishe mara moja na kwa upande wa wahamiaji haramu, waondoke nchini au wahalalishe ukazi wao kabla ya operesheni hiyo.

Hatua hiyo ya polisi inalenga kutekeleza agizo la Rais Jakaya Kikwete alilotoa akiwa mkoani Kagera juu ya wanaomiliki silaha isivyo haramu pamoja na wahamiaji haramu. Senso alisema operesheni hiyo itaendeshwa na polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama.

Kutokana agizo la Rais la kuwataka watu wote wanaomiliki silaha kinyume cha sheria kusalimisha silaha hizo, pamoja na watu wote wanaoingia ama kuishi na kufanya shughuli hapa nchini bila kufuata utaratibu kutakiwa kuondoka au kuhalalisha ukaazi wao, Jeshi la Polisi linawataka watu hao kuendelea kutekeleza agizo hilo la Serikali kabla ya operesheni kamambe kuanza,” ilisema taarifa hiyo. Hata hivyo Senso katika taarifa yake, alisema baadhi ya watu wamekwishasalimisha silaha wanazomiliki kinyume cha sheria na pia baadhi ya wahamiaji haramu wameanza kuondoka.

 Alisema mambo hayo yametekelezwa hususan katika mikoa ya Kagera na Kigoma. “Hiyo ni hatua nzuri, tunawataka wale wote ambao bado hawajatekeleza agizo hilo, waendelee kufanya hivyo haraka kabla ya muda wa msamaha kumalizika,” alisema Senso ambaye hata hivyo taarifa haikutoa idadi. Wakati huo huo Mrakibu Msaidizi wa Uhamiaji, Rosemary Mkandala alisema changamoto kubwa katika kukabili wahamiaji haramu ni ukubwa wa eneo la nchi, ambapo mikoa mingine imekuwa na vipenyo vingi.

Kwa mujibu wa Mkandala, Mkoa wa Kilimanjaro una vipenyo zaidi ya 400. Alisema wakati mwingine wananchi wamekuwa wakishindwa kutambua wahamiaji haramu kutokana na kuzungumza Kiswahili.

Alisema utoaji wa vitambulisho vya taifa utasaidia kwa kiasi kikubwa kuwatambua . Hata hivyo Mkandala ambaye alikuwa akizungumza na gazeti hili katika maonesho ya Nanenane, Dodoma, alisema elimu kwa umma imesaidia kupunguza tatizo la wahamiaji haramu na kutaka wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kuwabaini wanaoingia nchini kwa kutumia njia za panya.

No comments: