Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Saturday, April 13, 2013

Madaktari bingwa wapelekwa mkoani Kigoma

WANACHAMA na wananchi mkoani Lindi wametakiwa kujitokeza kwa wingi ili kutumia vyema fursa za huduma za madaktari bingwa zinazoratibiwa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) katika Hospitali ya Mkoa ya Sokoine.

Mwito huo umetolewa na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Lindi ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Abdallah Ulega wakati wa uzinduzi wa mpango maalumu wa utoaji huduma za matibabu kwa madaktari bingwa kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili.

Madaktari bingwa ni wa magonjwa ya akinamama, wataalamu wa upasuaji na magonjwa ya moyo,figo na shinikizo la damu.

Ni fursa adhimu ambayo wengi wetu hapa mkoani Lindi, hatukuwahi kukutana nayo na sababu kubwa inawezekana ni uwezo wa kugharimia safari ya kwenda huko wanakopatikana madaktari bingwa sanjari na mlolongo mrefu wa taratibu za kitabibu ili kuwafikia, lakini wenzetu, yaani Bodi ya Wakurugenzi, Menejimenti ya Mfuko wa Taifa ya Bima ya Afya wameiona changamoto hii na niseme wazi kuwa mpango huu utakuwa unaokoa maisha ya watu wengi ambao hawakuwahi wala kuwa na ndoto za kukutana na madaktari bingwa katika maisha yao," alisema Ulega.

Huduma hizo zimepangwa kufanyika kwa siku saba. Aidha Kaimu Mkuu wa Mkoa huo aliwataka madaktari wa Sokoine kushirikiana na madaktari bingwa kujifunza ili kujiongezea ujuzi wa kitabibu ili watakapoondoka huduma hizi zisitetereke bali ziboreke zaidi. Pia aliwataka wananchi kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ili waweze kunufaika kwa kupata matibabu.

Maradhi hayabishi hodi wananchi hivyo kwa kuchangia CHF uhakika wa matibabu ni mkubwa na pia utachochea maboresho ya huduma za matibabu kwenye vituo vya afya, zahanati hadi hospitali mkoa wetu" alisema Ulega.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Emanuel Humba alisema mpango huo maalumu wa kupeleka huduma za madaktari bingwa kwenye mikoa ya pembezoni , umezingatia mahitaji ya msingi na ya wakati kwani ni dhahiri wapo wanachama wetu wengi waliopo vijijini, wana mahitaji makubwa ya huduma za madaktari bingwa.

Alisema Mfuko umewagharimia madaktari hao pamoja na utoaji wa dawa na vifaa tiba, ili kufanikisha mpango huo wenye thamani zaidi ya milioni hamsini na mpango huu maalumu utekelezaji wake umeanzia mkoani Lindi na utakuwa ukitekelezwa kila baada ya miezi mitatu na wanachama wa Mfuko watapata matibabu kwa kutumia kadi zao sambamba na wananchi watapata huduma kwa kupitia utaratibu wa kawaida ambao utakuwa na nafuu.

Aliitaja mikoa ambayo iko kwenye mpango huu maalumu kuwa ni Kigoma, Rukwa, Katavi, Mara, Pwani na Tabora, hivyo wanachama na wananchi kwa ujumla wajitokeze ili waweze kutumia fursa hii muhimu na adimu kupata huduma za matibabu za madaktari bingwa.

No comments: