Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Thursday, July 12, 2012

Walimu walazimishwa kukopa Kigoma


WALIMU mkoani Kigoma wamezituhumu baadhi ya taasisi za fedha mkoani humo kwa kuwaingiza kwenye mikopo bila ridhaa zao na kufananisha na utapeli.

Mwenyekiti wa Katibu wa Chama cha Walimu Mkoa Kigoma, Saidi Ndee alisema yapo malalamiko ya walimu kuwa asasi hizo zimetafuta hundi namba za walimu bila wahusika kujua na kujikuta wakiwa kwenye mikopo jambo ambalo wengine hawakuwa tayari kuchukua mikopo hiyo.
Ndee alisema kuwa kitendo hicho ni sawa na uhuni ambapo ameitaka Serikali kuchukua hatua madhubuti katika kukomesha vitendo hivyo na kinyume cha maadili ya taasisi za fedha kinachofanywa na taasisi hizo.

Kulingana na taarifa hizo Katibu wa CWT Wilaya ya Kasulu, Lucy Masegenya aliwataka walimu wote ambao waliingizwa kwenye mikopo na taasisi hizo, ikiwemo ya Bayport bila ridhaa yao kuwasilisha vielelezo vyao ofisini kwake ili hatua za kisheria zichukuliwe.

Maseganya alisema kwa kiasi kikubwa taasisi hizo za fedha licha ya kufanya kitendo hicho kinyume na maadili ya taasisi za fedha, lakini pia zimekuwa zikitoza riba kubwa ambayo imekuwa mzigo mkubwa kwa walimu na mikopo hiyo kutokuwa na manufaa yoyote.

Sambamba na hilo Katibu huyo alisema taasisi hizo za fedha zimekuwa zikienda Hazina Ndogo mkoani humo na kuzungumza na watendaji wa ofisi hiyo, na kufanikisha mkakati wao wa kuwaingiza walimu kwenye mikopo bila ridhaa yao na kuanza kuwakata marejesho kila mwezi.
Meneja wa Bayport Mkoa Kigoma, Jackson Kakwaya alikanusha kuwepo kwa vitendo vya taasisi hiyo bila ridhaa yao.

Hata hivyo Meneja huyo amekataa kutoa maelezo kwa kile alichoeleza kuwa hana mamlaka ya kuisemea taasisi hiyo na badala yake alitaka jambo hilo aulizwe Mwakilishi Mkazi wa Bayport nchini aliyefahamika kwa jina la Mica ambaye hata hivyo simu yake haikupatikana.

No comments: