Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Tuesday, June 5, 2012

Mwakyembe amng’oa Bosi Mkuu ATCL baada ya kuanguka ile Ndege ya Kigoma




Paul Chizi, aliyekuwa Mkurugenzi wa ATCL

Ndege iliyodindoka ikitoka Kigoma kwenda Tabora

WAZIRI wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe ametengua uteuzi wa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL), Paul Chizi na kusimamisha kazi wakurugenzi wengine wanne wa kampuni hiyo.

Aidha, amemteua Kapteni Lusajo Lazaro, kuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni hiyo tangu jana
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Wizara hiyo jana, ilisema uteuzi huo umetenguliwa baada ya kubainika kuwa ulifanyika bila kufuata sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma.

Sheria ya mwaka 2002 na Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2003, inaelekeza bayana kuwa kama uteuzi utakuwa umefanyika kwa kukiuka sheria, utatenguliwa mara moja,” ilieleza taarifa hiyo. Wakurugenzi wengine waliosimamishwa kazi ni pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Uhandisi, John Ringo; Kaimu Mkurugenzi wa Fedha, Justus Bashara; Mwanasheria wa ATCL, Amini Mziray na Kaimu Mkurugenzi wa Biashara, Josephat Kagirwa.

Chizi aliteuliwa kukaimu nafasi hiyo Agosti 6 mwaka jana, baada ya aliyekuwa Mkurugenzi wake, David Mattaka kujiuzulu na baadaye kufikishwa mahakamani kwa kutumia vibaya madaraka na kuisababishia hasara kampuni hiyo.

Baada ya Chizi kushika nafasi hiyo, kampuni hiyo imekuwa ikiongeza idadi ya ndege na hivi karibuni ilizindua tovuti ikiwa ni katika jitihada za kutangaza huduma zake kwa wadau wa ndani na nje ya nchi. Kampuni hiyo imekuwa katika matatizo kadhaa ambapo hivi karibuni ndege yake aina ya Dash 8 Q300 ilishindwa kuruka na kuingia porini ikiwa na abiria 39 katika uwanja wa ndege wa Kigoma.

Ndege hiyo ilikuwa ikitoka Kigoma kwenda Tabora na baadaye Dar es Salaam na ilivunjika vipande kabla ya kikosi cha Zimamoto kufika na kudhibiti uwezekano wa kuteketea kwa moto.
Sababu za kushindwa kuruka, zilielezwa kuwa ni kutokana na matope yaliyokuwa kwenye njia ya ndege kuruka na kuifanya ipoteze mwelekeo.

Hata hivyo, baada ya kukaa muda bila ndege, hivi karibuni kampuni hiyo ilikodi ndege nyingine kutoka Dubai Boeing 737-500 ambayo imeanza kazi.
Mbali na kufanya kazi ikiwa na ndege moja, kampuni hiyo pia imekuwa ikijiendesha kwa ruzuku ya Serikali baada ya kukaa kwa muda mrefu bila kufanya biashara huku ikiingia gharama za kulipa wafanyakazi na nyingine za uendeshaji.

No comments: