Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Saturday, May 12, 2012

VETA watakiwa kuwa wazi katika udahili

SERIKALI imevitaka Vyuo vya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Nchini (VETA) kuwa wazi na kuweka matangazo kwenye vyombo vya habari kuhusiana na udahili mpya wa wanafunzi kujiunga na vyuo hivyo ili kuwafanya watu wengi zaidi kujua taratibu za kujiunga na vyuo hivyo.

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philipo Mulugo amesema hayo alipokuwa akizungumza na wakufunzi na watumishi wa Chuo cha VETA Kigoma alipokuwa kwenye ziara ya siku mbili mkoani humo kutembelea taasisi zilizo chini ya Wizara yake ambapo sambamba na hilo ametaka vyuo hivyo kutangaza sifa za wanafunzi wanaostahili kujiunga navyo.


Mulugo amesema kuwa kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi ambao wanaeleza kutaka kutumia fursa ya kupeleka watoto wao kupata mafunzo kutoka katika vyuo hivyo lakini taratibu za kujiunga na sifa za wanachuo limekuwa tatizo kubwa kwao.


Katika hatua nyingine Naibu Waziri huyo wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi ametangaza kutafuta popote walipo walimu zaidi ya 100 ambao wamepangiwa kufundisha mkoani Kigoma lakini hawakuripoti katika vituo vyao na badala yake kufanya ujanja na kubadilishiwa mikoa.


Awali Kaimu Mkuu wa Chuo cha VETA Kigoma, Alban Kisomba amesema kuwa chuo hicho kinakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo mkoa kukosa viwanda jambo linalowafanya wanafunzi kushindwa kufanya mafunzo kwa vitendo.


Ili kukabiliana na hali hiyo alisema kuwa wamelazimika kuwapeleka wanafunzi wa ufundi katika chuo hicho kwenye viwanda vilivyopo nje ya mkoa vinavyoendana na fani zao jambo ambalo ni gharama kubwa kwa wanafunzi na uongozi wa chuo.

No comments: