Karibu kwenye Blog ya Kijamii ya Kigoma yetu kwa habari na matangazo kwa bei nafuu sana. Tunakalibisha maoni, ushauri na habari zako ili tuijenge Tanzania kwa pamoja.

Saturday, May 12, 2012

Kigoma waonywa kutochezea mashine za kodi

MAMLAKA ya Mapato nchini (TRA), Mkoa Kigoma imewatahadharisha wafanyabiashara mkoani hapa kuachana na vitendo vya kuchezea mashine maalumu za kutoa risiti.

Kauli hiyo imetolewa na Meneja wa TRA Mkoa wa Kigoma, Augustino Mukandara.


Amesema katika mkutano wa siku moja wa Elimu kwa Walipa Kodi uliowajumuisha wafanyabiashara wa Manispaa ya Kigoma Ujiji kuwa kitendo cha wafanyabiashara kuchezea mashine hizo ni ukiukwaji mkubwa wa sheria.


Mukandara aliwaambia wafanyabishara hao kulipa kodi kwa hiari na kwa kuzingatia sheria ili kuiwezesha mamlaka ya mapato kukusanya mapato ya kutosha na kuiwezesha Serikali kuwa na mapato ya kutosha kugharimia shughuli mbalimbali za maendeleo nchini.


Aidha Meneja huyo wa TRA Mkoa wa Kigoma ametoa wito kwa wafanyabiashara mkoani Kigoma kutoa taarifa mapema kwa mawakala waliowasambazia mashine hizo na kuandika muda ambao mashine husika iliacha kufanya kazi ili kuepuka usumbufu usio wa lazima wa kisheria kwa mfanyabiashara kupewa adhabu.


Kwa upande wao wafanyabiashara katika Manispaa ya Kigoma Ujiji wamesema kuwa mkutano huo wa siku moja umekuwa na manufaa makubwa sana kutokana na kupata maelezo na maelekezo sahihi juu ya utumiaji wa mashine za risiti na kurudishwa kwa kodi ya ongezeko la thamani VAT.


Mmoja wa wafanyabiashara hao, Bernard Sadala alisema kuwa uwepo wa mashine hizo utawezesha Serikali kupitia TRA kukusanya kodi sahihi inayopaswa kulipwa na wafanyabishara.

No comments: